Mkuu wa mkoa wa Arusha awataka maafisa usafirishaji kuzingatia sheria za usalama barabarani

Maafisa usafirishaji wakimsikiliza Mkuu wa mkoa wa Arusha.

Mkuu wa mkoa wa Arusha,Amos Makalla akizungumza kwenye mkutano na maafisa usafirishaji wa abiria kwa kutumia Pikipiki na Bajaji mkoa wa Arusha uliofanyika kwenye viwanja vya Makumbusho.

Na Mwandishi Wetu,Arusha

Mkuu wa mkoa wa Arusha,Amos Makalla ametoa wito kwa maafisa usafirishaji wa Bodaboda na Bajaj kumwombea dua njema ili uteuzi utakapofanyika aendelee kuwa Arusha abadilishe sekta hiyo iwe ya kisasa kwa kuwapeleka viongozi wa umoja wao kujifunza kwa wenzao katika jiji la Kigali,Rwanda.

Ametoa kauli hiyo  wakati akizungumza na maafisa hao akiwa ameambatana na Wakuu wa wilaya zote sita  aliowaita kusikiliza changamoto zao katika utaratibu aliojiwekea wa kusikiliza wananchi katika makundi mbalimbali ili kuzipatia ufumbuzi wa haraka.

“Wakati mwingine sio vizuri kutoa ahadi ukiwa na furaha,mniombee kwa mwenyezi Mungu  mkeka ukitoka nami niendelee kuwepo Arusha,nitawapeleka baadhi ya viongozi wenu kwenye jiji la Kigali kujifunza kama nilivyofanya wakati nikiwa Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam na sekta hiyo ilibadilika,”

“Niliwaambia viongozi wenzangu wakati nipo mkoa wa Mbeya, hii kazi ya usafirishaji wa abiria kwa kutumia Pikipiki na Bajaj ni kazi kama zilivyo  kazi nyingine, wanafanya kazi muhimu ya kutunza familia zao pia ni wasomi wa ngazi mbalimbali hivyo itengenezewe mazingira mazuri ,”amesema Makalla

Amewakata wakuu wa wilaya za mkoa huo kuweka utaratibu wa kusikiliza kero za wananchi kwenye Kata zao na kupitia halmashauri za wilaya kuweka utaratibu wa kuwakopesha waendesha Bodaboda na Bajaj kama yalivyo makundi mengine wanaonufaika na mikopo ya asilimia 10.

Awali Katibu wa Umoja wa Bodaboda mkoa wa Arusha,Hakimu Msemo akisoma risala ya umoja wao amesema shughuli zao zinatoa mchango mkubwa kiuchumi kwa kutoa ajira kwa vijana na kupunguza ukosefu wa usalama kwenye jamii.

Mbali na kujikwamua kiuchumi ameongeza kuwa usafishaji huo unakuza sekta ya utalii wa ndani kutokana na madereva wa vyombo hivyo kuwafikisha wateja wao maeneo mbalimbali kwa haraka na wamekua wakishiriki shughuli za kijamii ikiwemo kufanya usafi kwenye vituo vya mabasi na hospitalini.

“Mkuu wa mkoa katika kipindi kilichopita tumeshuhudia mahusiano kati ya umoja wetu na serikali yakiimarika kwa kutambua kazi yetu na kuwaingiza kwenye mfumo wa kanzi data madereva kwenye vituo vyao ili watambulike kirahisi na kuepuka wasio na nia njema kujiingiza kwa manufaa binafsi,”amesema Msemo

Amesema licha ya mafanikio hayo zipo changamoto zinazowakabili zikiwemo kukosekana na vituo vya kudumu,ukosefu wa mafunzo ya udereva kwa baadhi ya watoa huduma,kuendesha pikipiki na Bajaj bila leseni na ukosefu wa mikopo rafiki ya kuboresha kazi zao.

Naye Katibu wa waendesha Bajaj mkoa wa Arusha,Salim Lyimo amesema umoja wao una wanachama 3,000 katika Jiji la Arusha ambao wamekua wakijipatia kipato cha kuendesha maisha yao lakini zipo changamoto zinazowakabili na kumwomba Mkuu wa mkoa azipatie ufumbuzi.

Amezitaja changamoto hizo kuwa ni kuondolewa kwenye vituo vyenye abiria wengi na kupelekwa sehemu ambako ambako hakuna abiria na miradi ya pamoja waliyokua wameianza kushindwa kuendelea baada ya kufutwa kwa vituo vilivyokua vinawaunganisha pamoja.

“Tunaomba vituo vya Bajaj vipangwe upya hasa maeneo yenye majengo makubwa,masoko,hospitali na vituo vya magari ili tuweze kufanya biashara,pia maeneo yasiyo na usafiri wa daladala ambayo ni Kijenge Juu,Ngusero,Lemara na maeneo mengine tupewe kipaumbe,”amesema Lyimo

Kwa upande wake Kiongozi wa waendesha Bajaj wenye mahitaji maalumu,Protas Ulomi ameshauri miundombinu ya Jiji la Arusha iboreshwe ili iendane na ongezeko la idadi ya watu pamoja na vyombo vya usafirishaji badala ya serikali kuchagua njia moja ya kuviondoa vyombo hivyo Katikati ya mji.

mwisho

 

Post a Comment

أحدث أقدم