Pages

April 20, 2018

BALOZI SEIF AKUTANA NA UONGOZI WA TAASISI YA FAWE

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na Taasisi za Kiraia katika kuona malengo na dhamira zilizojipangia katika kuwahudumia Wananchi zinafanikiwa vyema.
Alisema Taasisi nyingi za Kiraia zilizoanzishwa Nchini zimeonyesha mwanga wa matumaini katika kusaidia huduma za Kijamii hasa kwenye Sekta na miradi ya Elimu jambo ambalo Serikali inastahiki kujivunia na kuendelea kuzipa ushirikiano huo.
Balozi Seif Ali Iddi alitoa kauli hiyo wakati akizungumza na Uongozi wa Taasisi ya Kiraia ya kumjengea uwezo wa Kielimu Mtoto wa Kike na Mwanamke ya Forum for African women Educationalist {FAWE} hapo Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.
Alisema kundi kubwa la Wanawake hivi sasa tayari limeshaamka katika kufukuzia maendeleo hasa katika masuala ya Kielimu kupitia Taasisi za Kiraia jambo ambalo limewapa nafasi ya kushiriki katika makundi mbali mbali ya maamuzi katika maeneo yao.
“ Kazi kubwa iliyofanywa na FAWE imewezesha kutoa msukumo kwa kundi kubwa la wanawake kuamka katika kufukuzia maendeleo”. Alisema Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.
Alieleza kwamba Historia inaonyesha wazi jinsi gani Mwanamke alivyokuwa akikosa fursa kwa Karne nyingi zilizopita kutokana na mfumo dume uliokuwa ukitumika kuwanyima haki zao hasa katika fursa za Uongozi na Maamuzi ya msingi.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliipongeza Taasisi hiyo ya FAWE kwa kazi kubwa inayowajibika ya kumfinyanga Mtoto wa kike na Mwanamke katika kumjengea msingi mzuri wa kujiamini Kimaisha kupitia Elimu.
Balozi Seif alisema jambo hili linapendeza kwa kuwaona Wazazi wenyewe wameelimika na kutoa ushirikiano kwa watoto wao Kielimu. Hivyo aliupa matumaini Uongozi huo wa FAWE kwamba atafanya juhudi za makusudi kwa kuziomba Taasisi zilizoendelea kusaidia Miradi ya Maendeleo iliyoanzishwa na Taasisi hiyo.
Mapema Mratibu wa Taasisi ya Kiraia ya kumjengea uwezo wa Kielimu Mtoto wa Kike na Mwanamke ya Forum for African women Educationalist {FAWE} Bibi Hinda Abdulla Ajmin alisema Taasisi hiyo iliyoasisiwa mnamo Mwaka 2002 ililenga kumshajiisha Mtoto wa Kike na Mwanamke katika Elimu ili ajitambue.
Bibi Hinda alisema Fawe ilitekeleza Miradi Miwili mikubwa ya Tuseme katika kumjengea uwezo wa kujiamini Mtoto wa Kike katika harakati zake za Kimasomo pamoja na ule wa Stamp uliolenga kumjenga Mtoto wa Kike kupenda masomo ya sayansi.
Mratibu huyo wa FAWE Zanzibar alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba yapo mafanikio makubwa yaliyopatikana kupitia Miradi hiyo Miwili ambayo ilijumuisha jumla ya Skuli 150 za Sekondari Unguja na Pemba iliyokwenda sambamba na kufunguliwa kwa Klabu zilizojumuisha Watoto watano.
Bibi Hinda alifafanua kwamba Taasisi hiyo hivi sasa imepata changamoto kubwa katika kuendesha ratiba zake kiufanisi kutokana na wafadhili waliokuwa wakiiunga mkono kumaliza muda wao wa mkataba mnamo mwaka 2017.
Wakati huo huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alikutana na Viongozi wa Dini pamoja na wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Vijana, Wanawake na Watoto kuzungumzia Wimbi la vitendo vya udhalilishaji wa Kijinsia na kuangalia Mikakati ya kupambana na janga hilo.
Katika mazungumzo yao Viongozi wa Dini Sheikh Fadhil Suleiman Soraga, Sheikh Salim Mohammed Hassan na Padre Charles Nundu walisema Jamii imefikia pahali pa kuona aibu kiasi kwamba nguvu za pamoja zinahitajika katika kukabiliana na janga hilo la udhalilishaji.
Walisema Jamii bado ina usiri wa kutoa ushahidi kwa kesi za Udhalilishaji na hatma yake zinakuwa sugu katika utekelezaji wake na kupelekea kuchangia uvurugaji wa Amani ya Nchi kwa Watu kuamua kujichukulia hatua mikononi Mwao.
Walieleza kwamba yapo baadhi ya matukio ya Kisiasa katika maeneo tofauti Nchini yanayoambatanishwa na kesi za udhalilishaji jambo ambalo ni hatari kwa Amani ya Taifa na Watu wake.
Viongozi hao wa Kidini wamependekeza kuanzisha kwa Kampeni na Operesheni Maalum Mitaani ya kuwafichuwa wadhalilishaji wa Kijinsia kwa kuwapa fursa Wananchi kuwataja wahusika wa Vitendo hivyo ambao wanajuilikana katika maeneo yao.
Nao Viongozi wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Vijana, Wanawake na Watoto walisema Serikali kupitia Wizara hiyo tayari imeshazindua Mpango Mtambuka wa Miaka Mitano wenye lengo la kupambana dhidi ya vitendo vya Udhalilishaji wa Kijinsia Nchini.
Walisema Mpango huo unatoa fursa pana zaidi ya ushiriki wa kila mwana Jamii, Viongozi na hata Taasisi za Kiraia kutoa nguvu zao za pamoja katika azma ya kuona vitendo hivyo viovu vipakwisha au kupungua kwa kiasi kikubwa.
Viongozi hao wa Wizara inayosimmaia Wanawake na Watoto walifahamisha kwamba zipo dalili za mafanikio katika utekelezaji wa Mpango huo Mtambuka kuafuatia baadhi ya sheria kufanyiwa marekebisho ili kukidhi mahitaji ya sasa ya kukomesha tatizo hilo sugu.
Akitoa nasaha zake Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema vitendo vya udhalilishaji wa Kijinsia vinavyowaathiri zaidi Akinamama na Watoto vinaendelea pia kuidhalilisha Nchi na Jamii kwa ujumla.
Balozi Seif alisema Zanzibar hivi sasa imekumbwa na wimbi la Dawa za Kulevya ambalo limefikia hatua ya kuundiwa Taasisi ya kupapambana na changamoto hilo kiasi kwamba ipo haja pia ya kuangalia uwezekano wa kuunda Taasisi itakayosimamia masuala ya kupiga vita udhalilishaji wa Kijinsia.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi kati kati akizungumza na Uongozi wa Taasisi ya Kiraia ya kumjengea uwezo wa Kielimu Mtoto wa Kike na Mwanamke ya Forum for African women Educationalist {FAWE} hapo Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar. Wa kwanza kutoka kushoto ni Mratibu wa FAWE Bibi Hinda Abdullah Ajmin na wa kwanza kutoka Kulia ni Mshika Fedha wa FAWE Bibi Sabra Issa Mohammed.
Mratibu wa Fawe Bibi Hinda Abdullah Ajmin Kushoto akimfafanulia Balozi Seif Miradi mbali mbali iliyoanzishwa na Taasisi hiyo ambayo tayari imeshamsaidia Mtoto wa Kike kujikomboa Kielimu.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alizungumza na Viongozi wa Dini pamoja na wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wazee, Vijana, Wanawake na Watoto kujadiliana Wimbi la vitendo vya udhalilishaji wa Kijinsia na kuangalia Mikakati ya kupambana na janga hilo. Picha na – OMPR – ZNZ

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...