Pages

June 30, 2017

SERIKALI KUJENGA SHULE YA MFANO KWAAJILI YA WALIMU WANAOFUNDISHA ELIMU MAALUMU

Naibu Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia,Mhandisi Stella Manyanya(kulia)akimsikiliza Mwalimu wa Shule ya msingi Bwawani wilaya ya Karatu mkoa wa Arusha,Zaina Thabiti wakati akikagua maonesho ya zana za kufundishia wakati akifunga mafunzo ya siku 10 ya walimu wa elimu jumuishi kutoka mikoa sita nchini yaliyofanyika katika Chuo cha Elimu Maalumu Patandi,Tengeru mkoa wa Arusha .Picha na Filbert Rweyemamu




Naibu Waziri wa Elimu,Sayansi na Teknolojia,Mhandisi Stella Manyanya  amesema serikali imeshaanda ramani na fedha Sh 1 bilioni kwaajili ya ujenzi wa Shule  ya mfano yenye ubora itakayotumika kwaajili ya mazoezi kwa walimu wa elimu maalumu katika Chuo cha Ualimu Patandi.

Akizungumza wakati akifunga mafunzo ya walimu wa elimu jumuishi katika Chuo cha Walimu Maalumu Patandi wilaya ya Arumeru ,Mhandisi Manyanya alisema serikali inatambua umuhimu wa kuwaelimisha wenye ulemavu na imeamua kuwekeza katika Chuo hicho ili kisaidie kuzalisha walimu wenye maarifa.

Jumla ya walimu 187 kutoka mikoa sita ya Mara,Singida,Arusha,Manyara, Tanga na Kilimanjaro walipewa mafunzo maalumu kwa siku 10  kuwawezesha kumudu kuwafundisha vyema watoto wenye matatizo ya akili na usonji .

Alisema serikali ya awamu ya tano imedhamiria kutatua changamoto hizo na katika bajeti ya mwaka wa fedha 2017/10 imeondoa kodi zote kwa wawekezaji watakaoanzisha viwanda kwaajili ya kutengeneza vifaa vya watu wenye mahitaji maalumu nchini.

Mhandisi Manyanya alisema kama taifa bado linakabiliwa na changamoto mbalimbali za utoaji wa elimu maalumu kutokana na jamii kutokua na uelewa wa watu wenye mahitaji maalumu ikiwemo ulemavu wa akili na usonji.

Changamoto nyingine aliyoitaja ni kuendelea kuwa na uwekezaji usiozingatia watu wenye mahitaji maalumu hasa katika miundombinu huku walimu walio wengi kukosa mafunzo kwaajili ya watoto wenye mahitaji maalumu na elimu jumuishi.

Alisema tayari serikali imenunua vifaa kwaajili ya kujifunzia na kufundishia watoto wenye mahitaji hayo vyenye thamni ya Sh 3.6 bilioni vitakavyosambazwa shule mbalimbali zitakazopokea wanafunzi wenye mahitaji maalumu.

"Sitakubali huu ufisadi uendelee haiwezekani walimu wa masomo ya kawaida wapewe mafunzo maalumu kwaajili ya mahitaji yaliyopo na wanaporudi kwenye halmashauri zao wanapangiwa kufundisha vipindi vya awali huu ni ufisadi dhidi ya rasilimali ya watu wenye ulemavu,"alisema Mhandisi Manyanya

Alisema mpango wa wizara yake ni kuanza kuwatambua walimu wote wenye elimu maalumu na kuwapangia kazi kwenye vituo vyenye watoto wenye matatizo ya akili na usnji ili wayatumie vyema maarifa waliyoyapata.

katika hatua nyingine alisema katika bajeti ya mwaka wa fedha wa 2017/2018 serikali imetenga Sh 1 bilioni kwaajili ya ujenzi wa kituo cha kisasa kwaajili ya mafunzo ya walimu eneo la Patandi mkoa wa Arusha.

Awali Mratibu wa mafunzo hayo,Ahiadu Sangoda alisema jumla ya vituo vinne nchi nzima vimetoa mafunzo kwa walimu 710 lengo likiwa kuwajengea maarifa,stadi na mwelekeo wa kufundisha wanafunzi wenye ulemavu wa akili na wenye usonji kwa umahiri mkubwa.


No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...