Pages

May 14, 2013

RAIS OBAMA NA WAZIRI MKUU WA UINGEREZA WAMKOMALIA PUTIN KUHUSU SYRIA


Rais wa Marekani,Baraka Obama na Waziri Mkuu wa Uingereza,David Cameron

Marekani na Uingereza zimeongeza shinikizo kwa Urusi juu ya mgogoro wa Syria, lakini rais Barack Obama ameonya kuwa hakutakuwa na suluhisho la haraka la mgogoro huo, huku jeshi la Assad likipata mafanikio zaidi.
Obama na waziri mkuu wa Uingereza David Cameron walitaka kujenga hamasa mpya nyuma ya mkutano wa kimataifa wa Syria unaodhaminiwa na Marekani na Urusi, ambao sasa unatarajiwa kufanyika mwezi Juni, wakati wawili hao walipokutana mjini Washington.
Cameron, akiwa ndiyo amekamilisha ziara nchinin Urusi, alisema anaamini London, Washington na Moscow wamepata muafaka juu ya mgogoro wa Syria, ambao umegharimu maisha ya maelfu ya watu. Obama alisema Urusi ina maslahi na wajibu wa kusaidia kukomesha mgogoro huo, akisema alikuwa amewasilisha ujumbe kwa rais Vladmir Putin kabla ya ziara ya waziri wake wa mambo ya kigeni mjini Moscow wiki iliyopita.
Hali bado ni ngumu sana Syria
Lakini, Obama alionya kuwa itakuwa vigumu sana kuishawishi Urusi kubadilisha msimamo wake, na kubainisha kuwa bado kuna tofauti za msingi kati ya nchi hiyo na mataifa ya magharibi. Obama alisema hata kama Urusi itashawishika na kusimama upande wao, hali nchini Syria bado ni ngumu sana kutokana na ushiriki wa Iran, kundi la Hezbollah na wapiganaji walio na mafungamano na mtandao wa Al-qaeda katika mgogoro huo.
"Siahidi kuwa kutakuwepo na mafanikio. Ukweli ni kwamba miungu ya ghadhabu ikishaachiwa katika hali kama tunayoshuhudia nchini Syria, inakuwa vigumu sana kuweka tena mambo sawa," alisema Obama.
Cameron aonyesha matumaini
Kwa upande wake, waziri mkuu Cameron alikuwa mwenye matumaini zaidi, akisema anaamini London, Washington na Moscow zimefikia muafaka juu ya mgogoro huo. Cameron alisema kuwa historia ya Syria inaandikwa kwa kutumia damu ya raia wa nchi hiyo, huku dunia ikitizama tu, na kuongeza kuwa wakati umefika kwa dunia kuja pamoja na kukomesha umuagaji huu wa damu. Cameron pia aliahidi kuongeza msaada usio wa kijeshi kwa baadhi ya makundi ya waasi nchini Syria kwa mara mbili katika kipindi cha mwaka ujao.
"Kama hatuusaidii upinzani nchini Syria ambao tunautambua kuwa halali, na uliosaini tamko kuhusu mustakabali wa Syria yenye kidemokrasia, inayoheshimu haki za wachache, tusipofanya kazi na upande huo, basi tusishangae kuona makundi yenye itikadi kali yakizidi kuongezeka," alisema Cameron.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...