Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Zanzibar, Ndg. Abdi Mahmoud Abdi, amesema ziara zake katika majimbo 50 na matawi yake zinalenga kuimarisha uhai wa Chama, kusikiliza changamoto zinazowakabili wanachama na kuhamasisha utekelezaji wa Ilani ya CCM.
Ndg. Abdi ameyasema hayo wakati akiendelea na ziara za kukagua uhai wa CCM katika Tawi la Pita na Zako, Jimbo la Kijini, Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Amesema ziara hizo pia zinalenga kuhamasisha viongozi na wanachama wa CCM kuunga mkono juhudi zinazofanywa na viongozi wakuu wa Serikali katika kuleta maendeleo endelevu kwa wananchi.
Amesema CCM itaendelea kuisimamia Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuhakikisha inatekeleza kwa vitendo Ilani ya Chama, ikiwemo kuweka mazingira bora kwa wananchi, hususan wakulima wa mwani, kupata masoko ya uhakika yatakayowawezesha kuongeza kipato na kuboresha maisha yao.
Kwa upande wake, Katibu wa Idara ya Organisation wa CCM Zanzibar, Ndg. Omar Ibrahim Kilupi, amewataka wanachama wa CCM na wananchi kwa ujumla kulinda amani na utulivu uliopo nchini, akisisitiza kuwa amani ni tunu kubwa waliyoachiwa na viongozi na mababu waliotangulia.
Viongozi wa Jimbo la Kijini, akiwemo Mbunge na Mwakilishi wa Jimbo hilo, wamemuahidi Naibu Katibu Mkuu huyo kuendelea kusimamia na kutekeleza Ilani ya CCM kwa vitendo, sambamba na kuimarisha huduma za kijamii kwa wananchi.
Wamesema wataendelea kushughulikia maeneo muhimu kwa wananchi, ikiwemo upatikanaji wa maji safi na salama, kuboresha huduma za afya pamoja na kuendeleza michezo kwa vijana.
Katika ziara hiyo, Ndg. Abdi pia amepata fursa ya kumtembelea na kumjulia hali Ndg. Mwanakombo Mcha Mohammed, ambapo alimpa faraja na kumtakia afya njema.















إرسال تعليق