Sekretarieti
ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) imezitaka Nchi zote Wanachama kuongeza
umakini wa ufuatiliaji, kuimarisha ujiandaaji wa dharura, na kuongeza uratibu
wa mipakani kufuatia uthibitisho wa mlipuko mpya wa Ugonjwa wa Virusi vya Ebola
aina ya Bundibugyo (EVD) katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).
Mlipuko
huo ulithibitishwa mnamo tarehe 15 Mei, 2026 na Waziri mwenye dhamana ya Afya
ya Jamii, na kitovu chake kipo katika Mkoa wa Ituri mashariki mwa DRC,
unaopakana na Uganda na Sudan Kusini. Shughuli za ukabilianaji zinaongozwa na
Wizara ya Afya ya Jamii, Usafi na Ustawi wa Jamii ya DRC kwa usaidizi wa
washirika.
Ripoti
za awali zinaonyesha kuwa mlipuko huo unaathiri zaidi kanda za afya za Mongwalu
na Rwampara, kukiwa na visa vinavyoshukiwa vilivyoripotiwa pia huko Bunia,
makuu ya mkoa na kitovu kikubwa cha usafirishaji katika kanda hiyo.
Hadi kufikia tarehe 15 Mei 2026, takriban visa 246 vinavyoshukiwa na vifo 65
vilikuwa vimeripotiwa. Vipimo vya maabara vilikuwa vimethibitisha angalau
sampuli 13 chanya za Ebola kati ya 20 zilizopimwa, ikijumuisha vifo vinne
vilivyothibitishwa.
Mlipuko wa sasa ni mlipuko wa 17 wa Ebola kurekodiwa nchini DRC tangu ugonjwa
huo ulipotambuliwa kwa mara ya kwanza mnamo mwaka 1976 karibu na Mto Ebola.
Visa
viwili vya Virusi vya Ebola Bundibugyo, vinavyohusishwa na wasafiri kutoka DRC,
vimethibitishwa kimaabara nchini Uganda, huku kifo kimoja kikiripotiwa katika
jiji kuu la Kampala.
Naibu
Katibu Mkuu wa EAC anayesimamia Miundombinu, Sekta za Uzalishaji, Jamii na
Siasa, Andrea Aguer Ariik Malueth, alisema mlipuko huu mpya unasisitiza tishio
linaloendelea linalosababishwa na magonjwa yanayoweza kugeuka kuwa milipuko na
umuhimu wa mshikamano na ujiandaaji wa kikanda.
“EAC inaendelea kuwa macho na imejitolea kikamilifu
kuziunga mkono Nchi Wanachama katika kuimarisha ufuatiliaji, utambuzi wa
maabara, kuzuia na kudhibiti maambukizi, mawasiliano ya hatari na
ushirikishwaji wa jamii, hasa katika maeneo ya mipakani,” alisema.
Ariik aliongeza zaidi kuwa, kutokana na kiwango kikubwa
cha harakati za watu na bidhaa katika kanda yetu, ujiandaaji ulioratibiwa na
ushiriki wa haraka wa taarifa ni mambo muhimu katika kuzuia maambukizi ya
mipakani na kulinda afya na maisha ya Waafrika Mashariki.
EAC inazihimiza Nchi Wanachama kuamilisha mipango ya
ujiandaaji ya kitaifa na ya mipakani, kuimarisha ukaguzi na ufuatiliaji katika
vituo vya kuingilia, na kuhakikisha kuwa wafanyakazi wa afya na timu za
ukabilianaji wa haraka wana vifaa na wamepewa mafunzo ya kugundua na
kukabiliana na visa vyovyote vinavyoshukiwa.
EAC
inafanya kazi kwa karibu na wizara za afya za kitaifa, taasisi za kikanda,
Africa CDC, WHO na washirika wa maendeleo, wakiwemo Deutsche Gesellschaft für
Internationale Zusammenarbeit (GIZ) GmbH, Kreditanstalt für Wiederaufbau (KfW)
na Bernhard Nocht Institute for Tropical Medicine (BNITM), ili kuimarisha uwezo
wa kuzuia, kujiandaa na kukabiliana na magonjwa ya milipuko katika kanda nzima.
Hii ni
pamoja na uanzishaji wa haraka wa mtandao wa maabara zinazotembea za EAC ili
kusaidia ufuatiliaji wa mipakani kando ya mpaka wa DRC, huku UVRI likiwa Kituo
cha Kikanda cha Ubora cha EAC kinachofanya kazi kwa karibu na EAC na BNITM ili
kuimarisha ukabilianaji wa utambuzi wa maabara katika kanda hiyo.
Ugonjwa
wa Virusi vya Ebola ni ugonjwa mbaya na mara nyingi wa kifo unaoathiri binadamu
na wanyama wengine jamii ya nyani. Huambukizwa kwa kugusana moja kwa moja na
damu au majimaji mengine ya mwili ya watu walioambukizwa, nyuso na vifaa
vilivyochafuliwa, miili ya watu waliokufa kwa Ebola na wanyama walioambukizwa
kama vile popo na wanyama wengine jamii ya nyani.
Muda
wa ugonjwa kujipenyeza mwilini (incubation period) huanzia siku 2 hadi 21, na
watu walioambukizwa hawaambukizi wengine hadi pale dalili zinapoanza
kujitokeza.
Dalili
za mapema ni pamoja na homa ya ghafla, udhaifu mkubwa, maumivu ya kichwa,
maumivu ya misuli na koo kuuma, ikifuatiwa na kutapika, kuhara, maumivu ya
tumbo na, katika baadhi ya matukio, kutokwa na damu au michubuko isiyoelezeka.
Kulingana
na aina ya virusi na upatikanaji wa huduma bora za usaidizi, viwango vya vifo
vya visa vinaweza kuanzia asilimia 25 hadi zaidi ya asilimia 70.
Kwa
sasa hakuna matibabu yaliyoidhinishwa ulimwenguni kote kwa aina zote za virusi
vya Ebola, lakini huduma ya mapema ya usaidizi, ikijumuisha kuongeza maji
mwilini na matibabu ya dalili maalum, inaboresha sana nafasi ya kuishi.
Chanjo
na tiba zinapatikana kwa baadhi ya aina za virusi na zinaendelea kuchukua
nafasi muhimu katika kudhibiti milipuko.
Sekretarieti
ya EAC inaihimiza jamii kutulia, kutafuta taarifa kutoka vyanzo rasmi na
kuzingatia miongozo ya afya ya jamii. Jamii zinashauriwa kuepuka kugusana na watu wagonjwa na
mabaki ya miili ya binadamu, kunawa mikono mara kwa mara, na kuripoti dalili
zozote zinazoshukiwa mara moja kwa mamlaka za afya.

Post a Comment