EAC INAZIHIMIZA NCHI WANACHAMA KUIMARISHA UJIANDAAJI BAADA YA MLIPUKO MPYA WA EBOLA NCHINI DRC

 

 

Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) imezitaka Nchi zote Wanachama kuongeza umakini wa ufuatiliaji, kuimarisha ujiandaaji wa dharura, na kuongeza uratibu wa mipakani kufuatia uthibitisho wa mlipuko mpya wa Ugonjwa wa Virusi vya Ebola aina ya Bundibugyo (EVD) katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC).

 

Mlipuko huo ulithibitishwa mnamo tarehe 15 Mei, 2026 na Waziri mwenye dhamana ya Afya ya Jamii, na kitovu chake kipo katika Mkoa wa Ituri mashariki mwa DRC, unaopakana na Uganda na Sudan Kusini. Shughuli za ukabilianaji zinaongozwa na Wizara ya Afya ya Jamii, Usafi na Ustawi wa Jamii ya DRC kwa usaidizi wa washirika.

 

Ripoti za awali zinaonyesha kuwa mlipuko huo unaathiri zaidi kanda za afya za Mongwalu na Rwampara, kukiwa na visa vinavyoshukiwa vilivyoripotiwa pia huko Bunia, makuu ya mkoa na kitovu kikubwa cha usafirishaji katika kanda hiyo.


Hadi kufikia tarehe 15 Mei 2026, takriban visa 246 vinavyoshukiwa na vifo 65 vilikuwa vimeripotiwa. Vipimo vya maabara vilikuwa vimethibitisha angalau sampuli 13 chanya za Ebola kati ya 20 zilizopimwa, ikijumuisha vifo vinne vilivyothibitishwa.


Mlipuko wa sasa ni mlipuko wa 17 wa Ebola kurekodiwa nchini DRC tangu ugonjwa huo ulipotambuliwa kwa mara ya kwanza mnamo mwaka 1976 karibu na Mto Ebola.

 

Visa viwili vya Virusi vya Ebola Bundibugyo, vinavyohusishwa na wasafiri kutoka DRC, vimethibitishwa kimaabara nchini Uganda, huku kifo kimoja kikiripotiwa katika jiji kuu la Kampala.

 

Naibu Katibu Mkuu wa EAC anayesimamia Miundombinu, Sekta za Uzalishaji, Jamii na Siasa, Andrea Aguer Ariik Malueth, alisema mlipuko huu mpya unasisitiza tishio linaloendelea linalosababishwa na magonjwa yanayoweza kugeuka kuwa milipuko na umuhimu wa mshikamano na ujiandaaji wa kikanda.

 

“EAC inaendelea kuwa macho na imejitolea kikamilifu kuziunga mkono Nchi Wanachama katika kuimarisha ufuatiliaji, utambuzi wa maabara, kuzuia na kudhibiti maambukizi, mawasiliano ya hatari na ushirikishwaji wa jamii, hasa katika maeneo ya mipakani,” alisema.

 

Ariik aliongeza zaidi kuwa, kutokana na kiwango kikubwa cha harakati za watu na bidhaa katika kanda yetu, ujiandaaji ulioratibiwa na ushiriki wa haraka wa taarifa ni mambo muhimu katika kuzuia maambukizi ya mipakani na kulinda afya na maisha ya Waafrika Mashariki.

 

EAC inazihimiza Nchi Wanachama kuamilisha mipango ya ujiandaaji ya kitaifa na ya mipakani, kuimarisha ukaguzi na ufuatiliaji katika vituo vya kuingilia, na kuhakikisha kuwa wafanyakazi wa afya na timu za ukabilianaji wa haraka wana vifaa na wamepewa mafunzo ya kugundua na kukabiliana na visa vyovyote vinavyoshukiwa.

 

EAC inafanya kazi kwa karibu na wizara za afya za kitaifa, taasisi za kikanda, Africa CDC, WHO na washirika wa maendeleo, wakiwemo Deutsche Gesellschaft für Internationale Zusammenarbeit (GIZ) GmbH, Kreditanstalt für Wiederaufbau (KfW) na Bernhard Nocht Institute for Tropical Medicine (BNITM), ili kuimarisha uwezo wa kuzuia, kujiandaa na kukabiliana na magonjwa ya milipuko katika kanda nzima.

 

Hii ni pamoja na uanzishaji wa haraka wa mtandao wa maabara zinazotembea za EAC ili kusaidia ufuatiliaji wa mipakani kando ya mpaka wa DRC, huku UVRI likiwa Kituo cha Kikanda cha Ubora cha EAC kinachofanya kazi kwa karibu na EAC na BNITM ili kuimarisha ukabilianaji wa utambuzi wa maabara katika kanda hiyo.

 

Ugonjwa wa Virusi vya Ebola ni ugonjwa mbaya na mara nyingi wa kifo unaoathiri binadamu na wanyama wengine jamii ya nyani. Huambukizwa kwa kugusana moja kwa moja na damu au majimaji mengine ya mwili ya watu walioambukizwa, nyuso na vifaa vilivyochafuliwa, miili ya watu waliokufa kwa Ebola na wanyama walioambukizwa kama vile popo na wanyama wengine jamii ya nyani.

 

Muda wa ugonjwa kujipenyeza mwilini (incubation period) huanzia siku 2 hadi 21, na watu walioambukizwa hawaambukizi wengine hadi pale dalili zinapoanza kujitokeza.

 

Dalili za mapema ni pamoja na homa ya ghafla, udhaifu mkubwa, maumivu ya kichwa, maumivu ya misuli na koo kuuma, ikifuatiwa na kutapika, kuhara, maumivu ya tumbo na, katika baadhi ya matukio, kutokwa na damu au michubuko isiyoelezeka.


Kulingana na aina ya virusi na upatikanaji wa huduma bora za usaidizi, viwango vya vifo vya visa vinaweza kuanzia asilimia 25 hadi zaidi ya asilimia 70.

 

Kwa sasa hakuna matibabu yaliyoidhinishwa ulimwenguni kote kwa aina zote za virusi vya Ebola, lakini huduma ya mapema ya usaidizi, ikijumuisha kuongeza maji mwilini na matibabu ya dalili maalum, inaboresha sana nafasi ya kuishi.

 

Chanjo na tiba zinapatikana kwa baadhi ya aina za virusi na zinaendelea kuchukua nafasi muhimu katika kudhibiti milipuko.

 

Sekretarieti ya EAC inaihimiza jamii kutulia, kutafuta taarifa kutoka vyanzo rasmi na kuzingatia miongozo ya afya ya jamii. Jamii zinashauriwa kuepuka kugusana na watu wagonjwa na mabaki ya miili ya binadamu, kunawa mikono mara kwa mara, na kuripoti dalili zozote zinazoshukiwa mara moja kwa mamlaka za afya.

 

Post a Comment

أحدث أقدم