MWENGE WA UHURU WAIBUA MAPINDUZI YA NISHATI SAFI ARUSHA SEKONDARI

 

Na Filbert Rweyemamu, Arusha

Halmashauri ya Jiji la Arusha imepiga hatua kubwa katika utekelezaji wa Mpango wa Taifa wa Nishati Safi ya Kupikia (2024–2034) baada ya taasisi 25 kati ya 239 kufanikiwa kuachana na matumizi ya nishati chafu ikiwemo kuni na mkaa.

 

Hatua hiyo imebainika  wakati wa mbio za Mwenge wa Uhuru kitaifa mkoani hapa, ambapo Kiongozi wa Mbio hizo,Wazo Michael Mwang’onda alizindua rasmi mradi wa nishati safi katika Shule ya Sekondari Arusha iliyopo Kata ya Kati.

 

Akisoma taarifa ya utekelezaji mbele ya kiongozi huyo, Mkuu wa Shule hiyo, Lorna Christopher Nteles alisema mradi huo umegharimu jumla ya Shilingi 12 milioni fedha zilizotokana na mapato ya ndani ya shule hiyo.

 

Uchunguzi wa kiteknolojia na kimazingira uliofanywa shuleni hapo unaonyesha kuwa, kuhamia kwenye nishati safi kutaiwezesha shule hiyo kuokoa wastani wa miti 4,500 kwa mwaka (sawa na ekari 15 za misitu) ambayo hapo awali ingekatwa kwa ajili ya kuni za kulisha wanafunzi 1,000.

 

"Zamani tulikuwa tunatumia gharama kubwa kununua kuni na chakula kilichelewa kuiva. Moshi na masizi vilikuwa vinachafua mazingira na kuwasababishia wapishi wetu magonjwa ya macho na kikohozi. Sasa changamoto hizo hazipo tena," alisema Nteles.

 

Akizungumza mara baada ya kukata utepe wa uzinduzi, Kiongozi wa Mbio za Mwenge wa Uhuru Kitaifa,Wazo Michael Mwang’onda aliupongeza uongozi wa shule na kuutaka mikoa mingine kuiga mfano huo wa Arusha.

 

"Mwenge wa Uhuru unamulika mabadiliko chanya ya kimazingira. Shule ya Sekondari Arusha imeonyesha mfano wa kuigwa kwa kutumia mapato yake ya ndani kulinda misitu yetu na kuokoa afya za wapishi. Hili ndilo lengo la Rais Samia la kuifanya Tanzania kuwa ya kijani," alisema Mwang’onda.

 

Jiji la Arusha lina jumla ya taasisi 239 zinazolisha zaidi ya watu 100 kwa wakati mmoja, na juhudi za kuzihamisha zote kwenda kwenye nishati safi zinaendelea chini ya kauli mbiu ya Mwenge wa Uhuru: "Tanzania ni Yetu Sote, Tushikamane kwa Pamoja Kuleta Maendeleo." 

 

Mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2026 wilaya ya Arusha umekimbizwa na kupitia miradi Saba ambayo ipo katika Kata Saba za halmashauri ya Jiji la Arusha kwenye sekta ya maji, afya, barabara na ujasiriamali kwa makundi ya vijana yenye thamani ya Sh.3.9 bilioni.

 

Mkuu wa wilaya ya Arusha,Joseph Mkude alisema kuwa mwaka huu, utekelezaji wa shughuli za maendeleo utafanyika kupitia miradi saba inayotekelezwa katika wilaya hiyo.

 

Alieleza kuwa miradi hiyo imejikita katika kuboresha sekta muhimu za huduma za jamii na maendeleo ya kiuchumi, ikiwemo maji, afya, barabara na kuwawezesha vijana kiuchumi kupitia miradi ya ujasiriamali.


 

Aidha, aliongeza utekelezaji wa miradi hiyo unalenga kuongeza upatikanaji wa huduma bora kwa wananchi, kuchochea maendeleo ya kiuchumi na kuboresha ustawi wa jamii katika maeneo husika.

 

„Tunataka kuona vijana wanachangamkia fursa zilizopo katika wilaya yetu ya Arusha na mkoa wa ujumla wakinufaika kupitia mikopo inayotolewa na kuwa kielelezo kwa vijana wengine kujiajiri ili kukabiliana na changamoto ya ajira ambayo serikali imekua ikitumia mikakati mbalimbali kuwawezesha vijana,”alisema Mkude

 

Alisema  kuwa wilaya inaendelea kuweka mazingira wezeshi ili vijana wanufaike na fursa mbalimbali zinazopatikana katika miradi ya maendeleo inayotekelezwa na kwamba vijana wengi wameanza kujitokeza na kutumia fursa hizo, huku baadhi yao wakinufaika moja kwa moja kupitia miradi ya ujasiriamali na shughuli nyingine za kiuchumi.


 

Alisisitiza kuwa walionufaika wanawakilisha kundi kubwa la vijana na kwamba juhudi zinaendelea kuhakikisha idadi kubwa zaidi ya vijana inafikiwa na kushirikishwa katika programu hizo.


 

Miradi itakayotembelewa na mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka huu ni ujenzi wa tenki la maji la Lita 50,000 eneo la Kimindorosi,ujenzi wa Shule mpya ya Sekondari Kata ya Muriet eneo la Bondeni City,mradi wa kikundi cha Vijana eneo la Njiro wanaojishughulisha na usindikaji wa vyakula.


 

Miradi mingine ni kukagua jengo la Upasuaji kwenye Kituo cha Afya Kata ya Moivaro,mradi wa nishati safi ya kupikia katika Shule ya Sekondari Arusha,ufugaji wa kuku wa mayai unaotekelezwa na vijana wawili na mradi wa ujenzi wa barabara ya kilometa 1.5 eneo la Metejoo kwa Giriki ulioibuliwa na wananchi.

 


 Mmoja wa wa wakimbiza Mwenge wa Uhuru kitaifa akiwa ameshika Mwenge huo walipowasili Shule ya Sekondari Arusha.


 Kiongozi wa mbio za Mwenge wa Uhuru mwaka 2026,Wazo Michael Mwang’onda kushoto akimsikiliza Mkuu wa Shule ya Sekondari Arusha (Arusha Sec) wakati akieleza umuhimu wa matumizi ya nishati safi ya kupikia shuleni hapo.


 Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Jiji la Arusha,John Kayombo (kulia) pamoja na maafisa wengine wa serikali wakati Mwenge wa Uhuru ulipotembelea mradi wa nishati safi ya kupikia katika Shule ya Sekondari Arusha.


Wanafunzi wa Shule ya Sekondari Arusha wakionesha uzalendo wao wakati wa makaribisho ya Mwenge wa Uhuru.

Mkuu wa Shule ya Sekondari Arusha,Lorna Christopher Nteles akisoma taarifa ya Mradi wa Nishati Safi ya kupikia katika shule hiyo.

 

 

Post a Comment

أحدث أقدم