Shauku na hamasa ya kushiriki mbio za Yas Kili International Half Marathon (21kms) imeonekana wazi miongoni mwa wakazi wa mikoa ya Kaskazini, baada ya idadi kubwa ya watu kujitokeza katika vituo vya kuchukua kits (jezi, nambari na vifaa vingine vya washiriki).
Vituo vya Moshi na Arusha vimepokea idadi kubwa ya wadau wenye shauku kubwa ya kushiriki mbio hizo huku wengi wakiwa wametimiza hatua hiyo ya awali ili kuepuka usumbufu siku ya mbio. Wakizungumza na waandishi wa habari, kwa nyakati tofauti, baadhi ya wakazi walieleza furaha yao na matarajio yao kwa mashindano hayo
Ni mara yangu ya kwanza kushiriki Yas Kili International Marathon, na nimefurahi sana. Kwa kweli, mbio hizi zina faida nyingi katika mkoa wetu kiuchumi lakini kwa washiriki kama mimi najiweka fit kiafya na mwanzo wa kufahamiana na watu mbalimbali” alisema Ester Msale, mkazi wa Moshi.
Kwa upande wake, Juma Ally ambae ni mkazi wa Arusha alisema: “Leo nimewahi hapa ili kuhakikisha nachukua kit yangu mapema tayari kwa kushiriki kilomita 21. Kwa mwaka huu kwa kweli hamasa ni kubwa sana, na nina furahi kushiriki pamoja na maelfu ya wapenzi wa mbio kutoka mikoa mbalimbali.”
Kampuni ya Mawasiliano Yas, imeendelea kuhimiza wakazi kujiandikisha mapema na kuchukua kits (jezi) zao mapema ili kuepuka usumbufu siku ya mbio. Mbio hizi hutoa fursa ya kipekee kwa washiriki kujivunia kuungana na maelfu ya wapenzi wa michezo, huku wakishirikiana kuhamasisha maisha yenye afya na jamii yenye mshikamano.
Yas Kili International Half Marathon inaendelea kuwa moja ya mashindano yanayovutia zaidi nchini, ikijumuisha washiriki wa ndani na nje ya nchi.

Post a Comment