Mwenyekiti
wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu Prof. Norman Sigallla King
(aliyesimama) akizungumza na wananchi wa kijiji cha Kizengi (hawapo
pichani) kilichopo kata ya Kizengi wilaya ya Uyui mkoani Tabora baada ya
kukagua ufikishaji na upatikanaji wa huduma za mawasiliano vijijini
wakati wa ziara ya Kamati hiyo.
Mtendaji
Mkuu wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote Eng. Peter Ulanga(aliyesimama
mbele) akifafanua jambo mbele ya Kamati ya Bunge ya Miundombinu wakati
wa ziara ya Kamati hiyo ya kukagua upatikanaji wa huduma za mawasiliano
vijijini kwenye kijiji cha Mayamaya kilichopo Kata ya Zanka wilaya ya
Bahi mkoani Dodoma.
Meneja
wa Kampuni ya Simu ya TTCL Mkoa wa Tabora Bwana James Mlaguzi (wa
kwanza kulia) akitoa taarifa kwa wajumbe wa Kamati hiyo wakati wa ziara
yao ya kukagua upatikanaji wa huduma za mawasiliano viijini kwenye
kijiji cha Kizengi kilichopo kata ya Kizengi wilaya ya Uyui mkoani
Tabora.
Mjumbe
wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu Mhe. Mussa Ntimizi akisalimiana na
wananchi wa kijiji cha Kizengi kilichopo kata ya Kizengi wilaya ya Uyui
mkoani Tabora wakati wa ziara ya Kamati hiyo ya kukagua ufikishaji na
upatikanaji wa huduma za mawasiliano vijijini.
…………………
Kamati
ya Miundombinu ya Bunge la Jamhuri ya Muungano Tanzania inaendelea na
ziara ya kukagua ujenzi wa minara ya simu, ufikishaji na upatikanaji wa
huduma za mawasiliano vijijini na kwenye maeneo yasiyo na mvuto wa
kibiashara ili kuhakikisha kuwa wananchi wanapata na kutumia huduma za
mawasiliano kwenye maeneo mbali mbali nchini. Kamti hiyo imeendelea na
ziara yake kwenye mikoa ya Dodoma na Tabora ili kujiridhisha na utendaji
kazi wa Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) wa kufikisha mawasiliano
kwa wananchi.
Katika
ziara hiyo, Mtendaji Mkuu wa UCSAF Eng. Peter Ulanga amesema kuwa Mfuko
umetoa ruzuku kwa Kampuni ya simu ya TIGO kujenga mnara ili kufikisha
huduma za mawasiliano kwa wananchi. Mfuko umetumia zaidi ya dola za
marekani elfu arobaini na moja na mia tano (41,500) ambapo ni sawa na
zaidi ya shilingi milioni 85 kuipatia kampuni ya TIGO kujenga mnara
ambao sasa unahudumia zaidi wa wakazi 4,000 wa kijiji cha Mayamaya na
vijiji vingine vya kata ya Zanka wilaya ya Bahi mkoani Dodoma ambapo
walikuwa hawana huduma za mawasiliano na sasa wananufaika na uwepo wa
huu mnara na wanapata huduma za mawasiliano. Mnara huu ulikamilika mwezi
Machi mwaka jana na kuanza kutoa huduma ya mawasiiano kwa wananchi.
Naye
mwakilishi wa kampuni ya simu ya TIGO mkoa wa Dodoma mhandisi Hassan
Said Gimbo wa kampuni hiyo amewaeleza wajumbe wa Kamati ya Bunge ya
Miundombinu waliofanya ziara ya kukagua ujenzi wa minara, ufikishaji na
upatikanaji wa huduma za mawasiliano kuwa kampuni yao imekamilisha
ujenzi wa mnara na sasa unatoa mawasiliano kwa wananchi. Pia ameongeza
kuwa kampuni ya TIGO inafuatilia mara kwa mara kwenye eneo hilo na
kuhakikisha kuwa mawasiliano yanapatikana. “Tunajitahidi kwa kiasi
kikubwa kukarabati na kuhakikisha kuwa pale mawasiliano yanapopotea au
kuwa hafifu tunafanya haraka kuyarudisha”, amesema mhandisi Gimbo.
Naye
Mjumbe wa Kamati ya Bunge ya Miundombinu akizungumza kwa niaba ya
Kamati hiyo Mhe. Mussa Ntimizi ameipongeza Serikali kwa kutoa ruzuku kwa
kampuni za simu za mkononi kupitia UCSAF ili kufikisha huduma za
mawasiliano vijijini. Mhe. Ntimizi ameongeza kuwa kwa sisi wawakilishi
wa wananchi tunaotoka vijijini tunaelewa mahitaji na kiu ya wananchi ya
kupata mawasiliano kwenye makazi yao na umuhimu wa huduma nyingine za
mawasiliano. “Ukiangalia eneo kama hili halivutii kibiashara hivyo sio
rahisi kwa kampuni za simu kama hii ya TIGO kuja kuweka mnara wa simu
hapa” amesema Mhe. Ntimizi.
Tumepata
taarifa kuwa zaidi ya vijiji vitano vyenye wakazi zaidi ya watu 4,000
wanapata mawasiliano kupitia mnara huu wa TIGO. “Kwa wananchi zaidi ya
4,000 kukosa mawasiliano sio kitu kidogo na Mfuko huu unafanya kazi
kubwa ya kufikisha mawasiliano vijijini na Serikali inatumia gharama
kubwa kujenga minara ya simu za mkononi na kutoa huduma za mawasiliano
vijjijini, hivyo wahakikishe kuwa huduma za mawasiliano zinapatikana
muda wote”, amesema Mhe. Ntimizi.
Pia,
ametoa rai kwa kampuni za simu nchini kuboresha na kukarabati
miundombinu ya mawasiliano na minara yao ili wananchi waendelee kupata
mawasiliano muda wote kwa kuwa serikali inatoa fedha nyingi kwa maana ya
ruzuku na kuwapatia kampuni za simu ili ziweze kufikisha huduma za
mawasiliano kwa wanachi muda wote.
Amesema
kuwa huduma hizi zina gharama kubwa sana na wananchi hawajui gharama
kubwa ambayo Serikali imeingia kutengeneza mnara huu ambazo ni kodi zao
na hawaoni thamani ya Serikali kuwaletea huduma hii. Wananchi muendelee
kulinda miundombinu ya mawasiliano na kusiwepo na wizi wa mafuta ya
dizeli, mitambo na vitu vingine kwa kuwa Serikali inatumia gharama kubwa
kufikisha huduma za mawasiliano vijijini ambapo ujenzi wa mnara mmoja
unagharimu zaidi ya shilingi milioni 200, hivyo kila mwananchi awe
mlinzi wa mwenzake ili kulinda miundombinu hii ya mawasiliano.
Tunaipongeza
Serikali kwa kujenga mnara kwenye kijiji chetu kwa kuwa tunapata
mawasiliano na pale yanapokuwa hayapatikani yanakatika wataalamu wa
kampuni ya TIGO wanafika na kurekebisha hali hii, “hakuna mawasiliano ya
kampuni nyingine yoyote zaidi ya hii ya TIGO kwenye eneo hili”, amesema
mkazi wa kijiji cha Mayamaya, Bwana Emmanuel Konyanza kilichopo kata ya
Zanka wilaya ya Bahi mkoani Dodoma.
Katika
ziara hiyo ya Kamati kwenye kijiji cha Kizengi kata ya Kizengi iliyopo
wilaya ya Uyui mkoani Tabora, Meneja wa TTCL mkoa wa Tabora Bwana James
Mlaguzi ameihaidi Kamati hiyo kuwa wataongeza upana wa masafa ya TTCL
ili yaweze kufika kwenye vijiji vya mbali zaidi kwenye kata ya Kizengi
ndani ya kipindi cha miezi miwili kuanzia sasa. Naye Diwani wa Kata hiyo
Bwana Magindika Lugaira Masaga akizungumza kwa niaba ya wananchi mbele
ya wajumbe wa Kamati hiyo amesema kuwa hapo mwanzo wananchi walikuwa na
shida kubwa ya mawasiliano.
Bwana Masaga anawashukuru wajumbe wa Kamati hiyo kufanya ziara na wanategemea kuwa huduma za mawasiliano zitaongezeka na kuwa bora zaidi kwa kuwa mawasiliano ya minara ya kampuni nyingine sio mazuri sana bali wanategemea mnara wa Halotel pekee ambao una masafa marefu na kufikia wananchi walio wengi zaidi. hivyo mnara wa TTCL ukikamilika utasaidia kuwafikia wananchi wengi zaidi wa kata hii yenye vijiji saba na wakazi 23,534.
Bwana Masaga anawashukuru wajumbe wa Kamati hiyo kufanya ziara na wanategemea kuwa huduma za mawasiliano zitaongezeka na kuwa bora zaidi kwa kuwa mawasiliano ya minara ya kampuni nyingine sio mazuri sana bali wanategemea mnara wa Halotel pekee ambao una masafa marefu na kufikia wananchi walio wengi zaidi. hivyo mnara wa TTCL ukikamilika utasaidia kuwafikia wananchi wengi zaidi wa kata hii yenye vijiji saba na wakazi 23,534.
Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano
No comments:
Post a Comment