Pages

September 19, 2017

JAFFO: KONGWA NI ENEO LENYE UTAJIRI WA URITHI WA UKOMBOZI WA BARA LA AFRIKA

 Na Bearice Lyimo-MAELEZO, DODOMA
Naibu Waziri Ofisi ya Rais-TAMISEMI Suleiman Jaffo amesema kuwa Programu ya Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika (ALHP) una historia adhimu kati ya Tanzania na Afrika Kusini na itasaidia kuimarisha uhusiano uliopo kati ya nchi hizo mbili.
 
Mhe. Jaffo ameyasema hayo leo Wilayani Kongwa, Dodoma wakati wa ziara ya Makatibu Wakuu, Wakurugenzi na Watalamu wa Programu hiyo kutoka Tanzania na Afrika Kusini  kujionea maeneo yaliyotumika wakati wa  Ukombozi wa Bara la Afrika ikiwemo Afrika Kusini.  
 
“Nchi ya Tanzania na Afrika Kusini zina urafiki mkubwa na wa karibu kuliko nchi nyingine yeyote Afrika, hivyo kupitia Programu hii tutazidi kuimarisha udugu na uhusiano uliopo” amefafanua Mhe. Jaffo.
 
Ziara hiyo ilihusisha maeneo ya makaburi ya wapigania uhuru wa Afrika Kusini, Kambi walipokuwa wanaishi, mahandaki walipokuwa wanajihifadhi dhidi ya maadui pamoja na madarasa yaliyotumika kwa ajili ya mafunzo kwa wapigania uhuru. 
 
Akizungumzia ziara hiyo Katibu Mkuu Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Prof. Elisante Ole Gabriel amesema kuwa lengo la ziara hiyo ni kuona maeneo yaliyotumika wakati wa Ukombozi wa Bara la Afrika ikiwemo Afrika Kusini na kujadili jinsi ya kutunza maeneo hayo kwa ajili ya kizazi cha sasa na vizazi vijavyo.
 
Aidha, Prof. Elisante ameongeza kuwa ziara hiyo ina umuhimu kwa nchi zote ikizingatiwa Tanzania ndio ilikuwa kinara wakati wote wa harakati za ukombozi wa  Bara la Afrika hatua inayopelekea kuthamini mchango uliotolewa na Tanzania kwa kusaidia kwa hali na mali katika ukombozi wa wananchi wa Afrika Kusini.
 
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Kongwa Mhe. Deogratius Ndejembi ametoa wito kwa viongozi waliokuwepo katika ziara hiyo kutoka Afrika Kusini kuona umuhimu wa maeneo hayo ya kumbukumbu ya historia ya nchi yao kwa kuyatunza na kuyaendeleza kwa ajili ya vizazi vijavyo ili watambue mchango wa Watanzania katika Ukombozi wa Bara la Afrika.
 
Akiongea kwa niaba ya viongozi kutoka Afrika Kusini, Kaimu Mkurugenzi Mkuu wa Mawasiliano Serikalini Plumla Williams ameametoa wito kwa Serikali zote mbili kuwa suala la Ukombozi wa Afrika lifundhishwe shuleni ili kuweza kutunza na kuimarisha Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika.
 
Mbali na hayo Bi. Plumla kwa niaba ya Serikali ya Afrika Kusini ameahidi kuwa wataendeleza kasi ya utekelezaji wa programu hiyo ili uweze kuwa na tija kwa pande zote mbili.
 
Programu ya Urithi wa Ukombozi wa Bara la Afrika ina wajibu wa kukusanya, kuweka kumbukumbu, kuhifadhi na kukumbuka nakishi ya Urithi wa Afrika tangu harakati za kupigania Uhuru wa Afrika hadi Bara zima lililokombolewa.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...