Pages

March 4, 2015

WAFUGAJI WASHAURIWA KUWASOMESHA WATOTO WA KIKE


Na Ferdinand Shayo,Simanjiro.

Jamii ya Wafugaji imeshauriwa kutilia mkazo suala la kuwasomesha watoto wa kike badala ya kuwabagua na kuwaozesha katika mdogo jambo  linalozototesha  maendeleo ya jamii hizo.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro Grace Mbarouk amesema kuwa endapo jamii hizo zitahamasika na kuwapeleka watoto wa kike shuleni  jamii itapata ukombozi ikiwa ni pamoja na kuondokana na umasikini.

Akizungumza katika Uzinduzi wa Miradi ya Ujenzi wa Bwalo la Wanafunzi,Nyumba za walimu na madarasa katika shule ya sekondari  Emboreet  uliodhaminiwa na ECLAT Foundation,Grace ameitaka jamii ya wafugaji kuacha kasumba ya kuwabagua watoto hao na badala yake kuwapatia haki yao ya msingi ya kupata elimu ili wawe chachu ya maendeleo ya jamii.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Joel Bendera amewataka wazazi wote kuhakikisha kuwa wanawapeleka shule watoto waliofaulu kwenda kidato cha kwanza na iwapo watakaidi agizo hilo watachukuliwa hatua ,pia ameipongeza ECLAT Foundation kwa juhudi zao za kuisaidia jamii ya wafugaji iweze kupata elimu bora.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa ECLAT Foundation ,Peter Toima amesema kuwa taasisi yake imedhamiria kusaidia jamii ya wafugaji katika masuala ya elimu na pia kusaidia vikundi vya kinamama ili waweze kukua kiuchumi.
 
Beatrice Elias Mwanafunzi wa kidato cha pili katika Shule ya Sekondari Emboreet anaeleza changamoto zinazowakabili  katika jamii yake ikiwemo kupangiwa zamu ya kuchunga ng’ombe na kufanya kazi nyingine kiasi cha kukosa muda wa kujisomea na kurudi nyuma kitaaluma.

Mabadiliko ya teknolojia pamoja na hali ya hewa yanaisukuma jamii ya wafugaji kubadilika ili kuendana na wakati na mahitaji .Jamii za wafugaji hazina budi kujiendeleza kielimu na kupata maarifa yatakayowaletea maendeleo ya kijamii,kiuchumi na kisiasa.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...