Pages

November 5, 2014

MIE TENA MICHANGO YA HARUSI, HAPANA!


BAADA ya matukio ya harusi ya Jumamosi iliyopita natoa onyo ole wake atakayeniomba mchango wa harusi, sitaki utani. Labda kwanza nikueleze jinsi tulivyopata misukosuko sana kwenye uchangiaji wa ile harusi, maana siku hizi hakuna pa kukimbilia, kila asubuhi unaamshwa saa kumi na mbili na meseji kwenye simu;

“Ndugu rafiki na jamaa wa familia ya Pingapinga inakukumbusha kuwa harusi ya mtoto wao imekaribia hivyo mchango wako unahitajika”, baada ya wiki  meseji huwa kali zaidi;“Siku zinaisha kwa nini hautoi mchango, unajua familia ya Pingapinga ina shughuli ya harusi ya mtoto wao, toa upesi au la usitulaumu.”
Basi hizi meseji zilikuwa nyingi kuliko zile za kampuni yangu ya simu inayobuni namna ya kunitoa mkwanja kila wiki. Hatimaye nikatoa faini, maana nisiite mchango, maana mchango haulazimishwi.
Sasa Jumamosi ndiyo ikawa siku ya harusi, kadi nililetewa mapema , nikahakikisha koti langu la kuendea harusini nalicheki vizuri, maana haya makoti yanayokaa kabatini miezi ni muhimu kucheki vizuri maana unaweza kukuta panya kazalia kwenye mfuko halafu wakatimka kutoka  kwenye makazi yao wakati uko katikati ya kucheza mduara wa harusi.

Kweli tukaingia ukumbini viti vilikuweko swafi, meza zimepambwa kwa maua na MC alitukaribisha kwa maneno mengi yaliyojaa vichekesho visivyochekesha, au vichekesho vingine vimesharudiwa na kila MC hapa mjini halafu akawa analazimisha watu wapige vigelegele!

Yote bure watu walikuwa wamenuna maana hakukuwepo na dalili ya hata chupa moja ya kinywaji, ila ahadi kibao zikawa zinatolewa na MC, mara ‘Roli la bia linakuja toka breweries, mara shampeni leo inatoka Ufaransa kwa helikopta.”
Ghafla wahudumu waliovalia vikofia kichwani wakapitisha sambusa mojamoja kwa kila mtu, wakisindikizwa na MC akituhamasisha tule tufurahi na bwana harusi. Kwa kweli hela yangu ikaanza kuniuma, kwanza nililazimishwa kulipa, halafu sioni chochote hawa jamaa vipi?
Wakati ukumbi mzima ukiwa umeendelea kununa utadhani kikao cha msiba, MC akatuambia eti bwana harusi ana machache kabla ya kutuaga kwenda kupumzika na mkewe. Pamoja na kisirani tulikuwa na hamu kumsikia mshenzi huyu anataka kusema nini.
Bwana harusi akasimama hata suti aliyovaa ilikuwa haijamkaa sawasawa, akakohoa kidogo akaanza, “Asante MC, kwanza naomba nimshukuru Mungu kwa kumuumba mke wangu, kwa hilo Mungu uko juu, kiukweli hapa nimepata mke mtulivu, mpole asiye na makeke, yaani najisikia nina bahati sana.
“Naomba niwashukuru wakwe zangu kwa kukubali kupokea robo tu ya mahari na kuruhusu ndoa hii ifanyike. Pia nishukuru kwa zawadi zao za kitanda, godoro, kabati na makochi asante sana.  Naomba nimshukuru baba mwenye nyumba wangu kwa kukubali niwe na deni la kodi ya mwaka ili kufanikisha harusi hii, mzee upo juu.
“Naomba nitoe shukrani kwa bosi wangu kwa kunipa likizo fupi ili nikamilishe shughuli hii, pia wafanyakazi wenzangu kwa zawadi yenu ya jiko la gesi. Namshukuru mke wa kaka yangu kwa kutuazima gauni la harusi, na kaka yangu kwa suti hii niliyovaa. Natoa shukrani kwa mtengeneza keki, nitairudisha keki kwako kesho kama tulivyokubaliana.
“Nawashukuru wazazi wangu kwa kuja na kikundi cha ngoma toka kijijini, kweli kimeziba pengo la burudani katika harusi hii. Naishukuru kamati ya wazee wa kanisa kwa kufanikisha kumshawishi mke wangu aolewe na mimi, niwape aksante kwa akina mama jirani kwa kuja na sambusa mlizokula toka makwao ili kufanikisha harusi hii, mradi harusi hii ni furaha tupu. “MC wewe ni rafiki yangu nashukuru kwa kukubali tulipane kidogokidogo aksante sanaaaaa!

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...