Pages

January 21, 2018

Waandishi wa Habari wa Dodoma Kupewa Kipaumbele Katika Mafunzo ya Kuwajengea Uwezo.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dkt. Binilith Mahenge akifungua mkutano mkuu wa mwaka wa chama Chama cha Waandishi wa Habari Mkoa wa Dodoma uliofanyika mapema leo mjini Dodoma.
Mkurugenzi wa Idara ya Habari MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali Dkt. Hassan Abbasi akizungumza na wanachama wa Chama cha Waandishi wa Habari Mkoa wa Dodoma wakati wa mkutano mkuu wa mwaka wa chama hicho uliofanyika mapema leo mjini Dodoma.
Mkurugenzi wa Manispaa ya Dodoma Bw. Edwin Kunambi akizungumza wakati wa mkutano mkuu wa chama cha waandishi wa habari Mkoa wa Dodoma uliofanyika mapema leo mjini Dodoma.
Baadhi ya wanachama wa chama cha waandishi wa habari Mkoa wa Dodoma (Press Club) wakifuatilia mkutano huo mapema leo mjini Dodoma.
Mwenyekiti wa Chama Cha waandishi wa habari Mkoa wa Dodoma Bw.Herbet Chidawali akitoa maelezo mafupi ya namna chama hicho kinavyotekeleza majukumu yake kwa ufanisi pamoja na changamoto zinazokikabili kwa sasa.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Kondoa Bw. Khalifa Kondo akizungumza na wanachama wa chama cha waandishi wa habari Mkoa wa Dodoma (Press Club) wakati wa mkutano mkuu wa chama hicho uliofanyika mapema leo mjini Dodoma.



Na. Lilian Lundo – MAELEZO, Dodoma.

Serikali kupitia Idara ya Habari ya MAELEZO imesema itatoa kipaumbele kwa waandishi wa habari wa Dodoma kwa kuwapa mafunzo ya kuwajengea uwezo kutokana na mkoa huo kuwa na matukio mengi ya Kitaifa na Kimataifa pamoja na kutembelewa na wageni wa Kimataifa.

Hayo yameelezwa leo mjini Dodoma na Mkurugenzi wa Idara ya Habari MAELEZO na Msemaji Mkuu wa Serikali Dkt. Hassan Abbasi alipokuwa akiongea wakati wa Mkutano Mkuu wa Chama cha Waandishi wa Habari Kanda ya Kati (The Central Press Club (CPC)).

“Nawathibitishia kuwa Serikali sasa iko Dodoma, Dunia sasa inategemea kusikia mambo mengi kutoka Dodoma. Shughuli za Kitaifa na Kimataifa zitakuwa zikifanyika hapa Dodoma ,” alisema Dkt. Abbasi.

Amesema mkoa huo utakuwa unapokea wageni mbalimbali wa Kimataifa hivyo ni lazima waandishi wa habari wa mkoa huo wawe na uelewa wa mambo ya Itifaki na diplomasia ili kuwasaidia katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku.“Lazima tubadilike hata katika uvaaji wetu, kwani sasa tunaenda kukutana na viongozi wakubwa wa nchi na wa Kimataifa,” aliongeza Dkt. Abbasi.

Aidha amesema, Idara ya Habari MAELEZO itaandaa mafunzo mafupi katika maeneo mbalimbali ya tasnia ya habari ikiwemo masuala ya itifaki na mambo ya diplomasia ili kuwajengea uelewa waandishi hao.Hata hivyo, Dkt. Abbas amesema Idara yake itatafuta ufadhili kwa mabalozi mbalimbali yaliyopo hapa nchini ili waandishi hao wakajifunze namna vyombo vya habari vya Kimataifa vinavyofanya kazi.

“Mwaka 2017 tulifanikiwa kupata ufadhili wa ubalozi wa China na waandishi Kumi walienda China, Bado hatujajua ni waandishi wangapi watafanikiwa kwenda mwaka huu, lakini tutao kipaumbele kwa waandishi wa habari walioko Dodoma,” alisisitiza Dkt. Abbasi.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa CPC Habel Chidawali amesema waandishi wa habari walioko mkoani humo walikuwa na changamoto ya kutoweza kujiendeleza katika tasnia ya habari kutokana na vyuo vilivyopo mkoani humo kutokuwa na kozi ya masuala ya habari.

“Kama viongozi wa CPC tumetembelea baadhi ya vyuo vilivyopo mkoani hapa na kuvishawishi kuanzisha kozi ya masuala ya habari katika vyuo vyao. Vyuo vitatu vimetuahidi kuanzisha kozi hiyo mwaka huu,”alisema Chidawali.Amesema kuwa ni mategemeo yao kuwa, waandishi wengi watajiendeleza kwa mwaka huu jambo ambalo litawaongezea weledi katika kazi zao za kila siku hasa kwa kipindi hiki ambapo sasa Serikali yote ipo mkoani humo.

Mkoa wa Dodoma tayari umepokea viongozi wakuu wa nchi wawili yaani Makamu wa Rais mhe. Samia Suluhu Hassan na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa pamoja na Mawaziri, Manaibu Waziri na Watumishi wa Serikali zaidi ya 3000. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli anatarajia kuhamia mkoani humo muda wowote mwaka huu.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...