Mwenyekiti
wa Tume ya Utumishi wa Umma, Mheshimiwa Jaji (Mstaafu) Dkt. Steven J.
Bwana (pichani) amewataka watumishi wa umma kuhakikisha wanafanya kazi
kwa uadilifu na kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na Taratibu za Utumishi wa
Umma na kujiepusha na vitendo vya rushwa kwenye utekelezaji wa majukumu
yao.
Akizungumza
katika mahojiano maalum hivi karibuni, Dkt. Bwana amesema Tume katika
kutekeleza majukumu yake ya msingi ya ukaguzi wa rasilimali watu na
kushughulikia rufaa na malalamiko, imebaini kuwepo kwa ukiukwaji wa
Sheria, Kanuni na Taratibu miongoni mwa Watumishi wa umma, Waajiri,
Mamlaka za Ajira na Nidhamu.
Amesema
kuwa baadhi ya Watendaji Wakuu wanashindwa kuwachukulia hatua kwa
mujibu wa Sheria, watumishi wenye utendaji usioridhisha na wanaokiuka
maadili ya utumishi wa umma walio chini yao. Tatizo hili lipo zaidi kwa
baadhi ya Halmashauri zetu na Taasisi za Umma.
“Kumekuwa
na udhaifu mkubwa kwa baadhi ya Watendaji Wakuu ambao wameshindwa
kuchukua hatua za nidhamu mapema dhidi ya watumishi walio chini yao.
Utakuta mtumishi anatoweka tu kazini bila kutoa taarifa wala kuomba
ruhusa! Mtumishi kutokuwepo kazini kwa siku tano bila ruhusa wala sababu
za msingi adhabu yake ni kufukuzwa kazi. Inashangaza kuona mtumishi wa
umma hayupo katika kituo chake cha kazi kwa zaidi ya siku tano, siku 115
na Mwajiri wake hajui, wala hachukui hatua.” Amesema.
Hata
hivyo, Dkt. Bwana ameonyesha kutoridhishwa na hali ya utendaji kazi
katika baadhi ya Halmashauri. Alisema, “Rufani nyingi tunazopata
zinatoka huko, kuna haja ya kurekebisha mambo mengi sana hasa kwenye
Halmashauri zetu, hakuko sawa kwa upande wa usimamizi wa Rasilimali
watu. Kuna wizi kule, kuna matumizi mabaya ya fedha za umma na mali za
Halmashauri.
Japokuwa
Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali “CAG” anafanya kazi
nzuri ya ukaguzi wake na kutoa ripoti, sehemu fulani watu wanachukuliwa
hatua za kisheria, lakini hayo maeneo yanahitaji kusimamiwa kikamilifu
zaidi. Bado kuna mapungufu mengi sana” alisisitiza.
Dkt.
Bwana amesema kuna haja ya Watendaji Wakuu kupatiwa mafunzo
yatakayowawezesha kujielimisha, ili waweze kuzielewa Sheria, Kanuni na
Taratibu zilizopo na kuzizingatia wakati wote wa kutekeleza majukumu
yao.
“Tatizo kubwa tunaloliona kwenye Halmashauri kule kuna mambo mengine
yanafanyika kana kwamba Viongozi hawajui Sheria ama wanazijua ila
wanazipuuza, Pawe na utaratibu wa kuwapatia mafunzo ya aina fulani ya
mara kwa mara Viongozi na Watendaji Wakuu, yatakayowawezesha kufanya
kazi bila kuvunja Katiba, Sheria, Kanuni na Taratibu zilizopo. Vyuo vya
Mzumbe, Chuo cha Serikali za Mitaa-Hombolo na Chuo vya Utumishi wa Umma
vitumike, kwani vikitumika kikamilifu vitasaidia sana kupunguza matatizo
ya utumishi tunayoyaona”. Alisema Dkt. Bwana.
Kwa
upande wa Watumishi wa Umma alisema, kumekuwepo kwa tabia na mienendo
isiyofaa kwa baadhi ya watumishi wa umma, ambayo imesababisha
kuchukuliwa hatua stahiki za kisheria au za kinidhamu. Miongoni mwa
makosa yanayofanywa na Watumishi mara kwa mara na kusababisha
kuwachukulia hatua ni kufanya vitendo vinavyodhalilisha utumishi wa
umma, wengine kushindwa kutekeleza majukumu yao, uzembe uliokithiri na
kusababisha hasara kwa mwajiri, utoro kazini, wizi na kukiuka maadili.
“Kuna
tatizo sugu la Watumishi wa Umma, hasa vijana wanaotaka kujiendeleza
kwenda masomoni kutokufuata taratibu. Rufani nyingi zinazokuja kwetu
unakuta watumishi wamefukuzwa kazi kwa kosa la utoro, wanapokata Rufaa
wanajitetea kuwa walikwenda masomoni. Hili ni tatizo sugu, vijana wana
haki ya kujiendeleza lakini pia kuna haki ya kufanya kazi mwajiri hawezi
kuruhusu watumishi wote wakaondoka kwenda masomoni bila kufuata
utaratibu wa mafunzo, wafuate utaratibu” alisema.
Akizungumzia
hatua mbalimbali zinazochukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano kwa
Watumishi wa Umma, mfano kwa upande wa watumishi wa umma waliopatikana
na vyeti vya kughushi alisema,
“Kughushi ni kosa, kosa la jinai, Sheria iko wazi, mtu yeyote
akituhumiwa kuwa na cheti cha kughushi akipelekwa Mahakamani anahukumiwa
na kupewa adhabu stahiki. Naipongeza Serikali kwenye hili. Mfano mdogo
umejitokeza kwenye usaili wa nafasi za kazi katika Afrika ya Mashariki,
mara nyingi vyeti vyetu Watanzania haviaminiki, wanachukuliwa wa kutoka
Kenya, Uganda na sisi kubaki kulalamika, wakati tunashindwa kushindana
kwenye soko la ajira.
Sawa,
unakuta mtu anaweza kuongea Kiingereza lakini cheti kinakuwa na
mashaka, ni asilia kweli hiki?. Ni vizuri mtu akapata mafanikio
kutokana na juhudi yako, siyo hizi njia za mkato mkato. Hapana, ni
zoezi ambalo nafikiri liendelee” alisema.
“Serikali ya Awamu ya Tano inafanya vizuri, tunaelekea kuzuri,
inapambana kurudisha nidhamu na kudumisha Maadili Serikalini. Udokozi
umepungua na Nidhamu ya kazi inarudi” alisisitiza.
Alitaja
miongoni mwa changamoto zinazoikabili Tume ya Utumishi wa Umma kuwa ni
uwezo mdogo wa kuzifikia Taasisi zote za umma kupitia jukumu la ukaguzi
wa Rasilimali watu ambao utasaidia kurekebisha kasoro nyingi
zitakazobainika na pia utoaji wa huduma. Hata hivyo, aliishukuru
Serikali kwa kuendelea kuiwezesha Tume ili iweze kutekeleza majukumu
yake.
Dkt. Bwana alihitimisha kwa kuwakumbusha watumishi wa umma kuwa
wanapaswa kuzingatia Maadili ya Utumishi wa Umma na ya Taaluma zao
wakati wote wanapotekeleza majukumu yao.
Imeandaliwa na:
KITENGO CHA MAWASILIANO SERIKALINI
TUME YA UTUMISHI WA UMMA
17 AGOSTI, 2017
No comments:
Post a Comment