Pages

March 30, 2015

JENERALI MWAMUNYANGE: MAMLAKA ZA MISHENI ZA ULINZI WA AMANI ZIWE WAZI


Na Mwandishi Maalum, New York
Mkuu wa Majeshi ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jenerali Davis Mwamunyange, amelishauri Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa, kuweka bayana na kwa uwazi mamlaka ( mandate) ambayo misheni ya kulinda Amani itapaswa kutelekeza kule inakopangiwa kwenda.
Ametoa ushauri huu siku ya Alhamisi wakati alipokuwa akitoa mchango wake kwenye mkutano wa Wakuu wa Majeshi ya Ulinzi ambao nchi zao zinachangia katika operesheni za ulinzi wa Amani za Umoja wa Mataifa.
Katika mkutano huo uliokuwa wa siku moja, na kuhudhuriwa na Wakuu wa Majeshi na Maafisa wa Ngazi za Juu ,kutoka nchi 108, Jenerali Mwamunyage amesema;
“ Wakati wa utoaji wa idhini na mamlaka kwa misheni ya kulinda Amani, Baraza Kuu la Usalama la Umoja wa Mataifa, linatakiwa kumwita mbwa kwa jina lake kama lilivyo.Mbwa aitwe kwa jina lake. Elezeni bayana na kwa uwazi mamlaka na idhini za utekelezaji za ya misheni ”
Na kuongeza, “ iwekwe wazi, kama ni misheni ya kulinda Amani, basi ielezwe ni ya kulinda Amani, na kama ni ya matumizi ya nguvu basi na iwe hivyo”. Amesisitiza Mkuu wa Majeshi
Amesema kwamba, kwa kutamka jina halisi /mamlaka ya misheni pale inapoundwa, Baraza Kuu la Usalama linakuwa linapeleka ujumbe ulio sahihi kwa pande zote zinazohusika pamoja na nini wakitarajie.

Jenerali Mwamunyage ameuleza washiriki wa mkutano huo mkutano wa kwanza wa aina yake kuwakutanisha Wakuu wa Majeshi zaidi ya mia moja, wakati mmoja na mahali pamoja. Kwamba, uwazi huo pia utasaidia kuweka bayana hatua za utekelezaji zinazofanywa na walinzi wa amani kwenye eneo la utekelezaji.

Vile vile Mkuu wa Majeshi ya Tanzania ameshauri pia kuwa misheni ambayo tangu kuundwa kwake zilikuwa na mamlaka ya kutumia nguvu, ni vema zisiendelee kutambuliwa hivyo pale mamlaka ya misheni hiyo yanapobadilika kutoka matumizi ya nguvu na kuwa misheni ya kulinda Amani au jina lolote lile.

Tanzania inawanajeshi wake katika Misheni mbalimbali ikiwa ni pamoja na UNAMID ( Darfur) UNFIL, ( Lebanon) MONUSCO ( DRC) na katika maeneo mengine. Vile vile Tanzania ina Polisi na Askari Magereza ambao nao wanahudumu katika misheni mbalimbali.

Akizungumzia kuhusu mkutano huo ambao ulifunguliwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa na Ban Ki Moon na kufungwa na Naibu Katibu Mkuu Jan Eliasson. Jenerali Davis Mwamunyange amesema, mkutano kama huo unapashwa kuitishwa mara kwa mara kwa kuwa unawawezesha wakuu wa majeshi kubadilishana uzoefu wao katika utekelezaji wa operesheni za ulinzi wa Amani na hasa kwa kuzingatia kwamba nchi wanachama ndio wanaotoa wanajeshi wao na ndio haswa wanaokumbana na changamoto mbalimbmali za utekelezaji wa dhamana hiyo.

Awali akifungua mkutano huo, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon pamoja na kuwashukuru Wakuu hao wa Majeshi kwa mchango wao katika eneo hilo la ulinzi wa Amani, amesema operesheni ya kulinda Amani chini ya Umoja wa Mataifa, licha kwa kwamba ni dhamana inayohitajika sana lakini pia inakabiliwa na changamoto mbalimbali.

Akazitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni upugufu wa raslimali fedha, zana, vifaa na teknolojia za kisasa lakini pia ugumu na hatari wanazokumbana nazo walinzi wa Amani, ambapo hivi sasa mbinu za kigaidi na uvamizi kwa walinzi wa Amani ni baadhi ya changamoto na hatari wanazokumbana nazo.

Katibu Mkuu, amewataka wakuu hao wa majeshi kuongeza ushirikiano wao kwa Umoja wa Mataifa na hasa katika kutafuta mbinu za kukabiliana na changamoto za kiulinzi na kiusalama ambazo duni hivi sasa inakabiliana nao.

Akaongeza kuwa kujitokeza kwa idadi kubwa ya wakuu hao wa majeshi ya ulinzi kushiriki mkutano huo, kumeipa faraja kubwa Umoja wa Mataifa.

Naye Naibu Katibu Mkuu Jan Eliasson, akihitimisha mkutano huo, amewataka wakuu hao wa majeshi na serikali zao kuendelea na majadiliano ya mchakaTo wa kuundwa kwa majeshi ya ulinzi ya kikanda, majadiliano ambayo yanatakiwa kuendelea kuelekea mkutano wa Operesheni ya Ulinzi wa Amani utakaofanyika mwezi Septemba mwaka huu.

Wakuu hao wa Majeshi ya Ulinzi pamoja na kutoa mchango wa mawazo yao, pia walipata fursa ya kupata maelezo kutoka kwa Viongozi wakuu waandamizi wanaoongoza Idara zinazozohusu Operesheni ya Ulinzi wa Amani.
------------------------------------------------------- 
HABARI KATIKA PICHA 

" Mnatuwakilisha vema?" ndilo swali ambalo Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Mwamunyange alilowauliza watanzania hawa wawili, Afisa wa Usalama wa UN Bw. Jacob Mwashiozya na Bw. Joseph Msami, wa Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa walipokuwa wakisalimiana naye na ujumbe wake mara baada ya kumalizika kwa mkutano wa wakuu wa majeshi ya ulinzi

Jenerali Davis Mwamunyange (watatu kushoto), akiwa na ujumbe wake mbele ya bendera ya Tanzania, baada ya kumalizika kwa mkutano wa siku moja wa Wakuu wa Majeshi ya Ulinzi kutoka nchi 108. Kutoka kushoto ni Kanali Adolf Mutta, Brigedia Jenerali Luwogo, Brigedia Jenerali Kamunde, Meja Ngh'abi, na Luten Kanal Itang'are

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Ban Ki Moon, akiingia kwa staii ya aina yake wakati alipokwenda kufungua mkutano wa kwanza wa aina yake kufanyika katika Umoja wa Mataifa, ambapo Wakuu wa Majeshi ya ulinzi kutoka nchi zaidi ya 100 walikutana kwa wakati mmoja na mahali pamoja kujadiliana na kubadilishana mawazo kuhusu operesheni za ulinzi wa amani za umoja wa mataifa.

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...