Pages

August 17, 2014

KIFO CHA MFANYAKAZI A TO Z CHAZUA UTATA

Songea.
Wakati mazishi ya aliyekuwa mfanyakazi wa kiwanda cha A to Z kilichopo jijini Arusha,Elias Sixmond Nditi(22) yaliyofanyika mwishoni  mwa wiki  nyumbani kwao eneo la Mji Mwema,Songea mjini mkoani Ruvuma ndugu wa marehemu wameapa kuchukua hatua za kisheria dhidi ya kiwanda hicho.
 
Mmoja wa ndugu wa marehemu ambaye ni pacha wa Mama mzazi wa Elias,Mary Nditi alisema kifo hicho kimewastua mno kutokana na kumfahamu  vema marehemu kutokuwa na tabia za ulevi.
 
“Huyu ni mwanangu niliyemlea baada ya pacha mwenzangu,Lucia Nditi kufariki dunia mwaka 2001,wakati akiwa hapa hatukuwahi kumuona akinywa Pombe ,labda alivyofika huko alianza ulevi hatuwezi kufahamu,lakini muda wa tukio tunaoambiwa alianguka kwenye Bwawa  ni saa 9 mchana ni jambo lisiloingia akilini,kwani hakuna uzio au ulinzi,"alisema Mary
 
Alisema walikuwa wakiwasiliana mara kwa mara na Elias kwa njia ya simu na kwamba aliwaambia kazi anazozifanya ni ngumu ukilinganisha na mshahara anaolipwa wa Sh 105,000 kwa mwezi na alikua akipanga kurejea nyumbani pindi akipata nauli.
 
Taarifa iliyotolewa na Polisi mkoani Arusha kwa vyombo vya habari ilisema tukio hilo lilitokea Agosti 12,mwaka huu kwenye kiwanda hicho baada ya mfanyakazi huyo kukutwa akiwa amefariki dunia kwenye Bwawa la kuhifadhia maji yanayotumika kiwandani hapo.
 
“Uchunguzi wetu wa awali unaonesha marehemu alionekana muda wa saa 9 alasiri akiwa eneo hilo la kiwanda huku akiwa amevua nguo na kukaa kwenye kingo za shimo hilo la kuhifadhia maji,baadaye hakuonekana  lakini nguo zake zikiwa kwenye kingo la Bwawa ndipo wafanyakazi wenzake waligundua alikuwa amekwishafariki dunia” ilisema taarifa ya polisi.
 
Hata hivyo ndugu mwingine wa marehemu aliyejitambulisha kwa majina ya Fransis Kahimba  alisema mwili wa ndugu yao baada ya kuuchunguza waliona ukiwa na jeraha kwenye jicho lake la kulia hali inayoonesha aligongwa na kitu chenye ncha kali.
 
Alisema wakati wakiwa kwenye lango la kuu la kiwanda hicho wakifatilia kifo cha ndugu yao walishangazwa na kauli zilizokuwa zikitolewa na wafanyakazi kuwa masuala ya vifo eneo hilo ni jambo la kawaida sana.
 
“Unajua hapo kiwandani kuna takribani wafanayakazi 9,000 ambao ukiwasikiliza shuhuda wanazotoa utashangaa kama haya mambo yanafanyika hapa Tanzania,na kama ni uwekezaji tuu ndio unafanyika au kuna mambo mengine yakiwamo ya ukiukwaji wa haki za binadamu na hakuna hatua za kisheria zinazochukuliwa,”alisema Kahimba
 

No comments:

Post a Comment

Related Posts Plugin for WordPress, Blogger...